Afrika

Habari

Burudani

Michezo

Biashara

Live Radio

Nchi

Kijamii

Lifestyle

SIL

DRC: Mapigano yameanza tena kati ya jeshi la Kongo na M23

ADF Yadaiwa Kufanya Mauji Ya Watu 42 DRC DRC: Mapigano yameanza tena kati ya jeshi la Kongo na M23

Mon, 9 Sep 2024 Chanzo: www.tanzaniaweb.live

Mapigano yameanza tena baada ya wiki tatu za utulivu mashariki mwa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo. Mapigano yaliripotiwa siku ya Jumapili, Agosti 25, kati ya jeshi la Kongo, likiungwa mkono na makundi ya ndani yenye silaha, na waasi wa M23 wanaoungwa mkono na Rwanda, katika eneo la Lubero kwenye barabara ya kaskazini wa mkoa wa Kivu Kaskazini.

Mapigano ya silaha nzito na kurushiana risasi yaliripotiwa siku ya Jumapili kati ya wapiganaji wa M23 na FARDC huko Kikuvo. Mapigano haya yalitokea kwenye barabara inayotoka Matembe kwenda Kirumba, kulingana na Luteni Kanali Mak Hazukay, msemaji wa operesheni za Sokola 1 Grand Nord.

Kulingana na shuhuda kutoka kwa wakazi, mapigano haya katika eneo la Lubero yalisababisha mvutano mkubwa karibu na mji wa Kirumba, eneo lililoko karibu kilomita mia moja kutoka mji wa Goma. "Sisi Wakongo lazima tuwe waangalifu na kuona jinsi ya kuchambua ukiukaji huu unaoendelea wa usitishaji mapigano," amesema Kanali Alain Kiwewa, mkuu wa kijeshi wa eneo la Lubero.

Kwa sasa, bado ni vigumu kujua ni nani anayedhibiti eneo hilo. Mashirika ya kiraia yanahofia kuendelea kwa mapigano kwenye barabara hii inayoelekea Butembo na Béni, miji miwili mikubwa na njia panda za kibiashara huko Kivu Kaskazini. Mapigano mengine pia yalitokea Rutshuru na katika eneo la Masisi.

"Kama serikali ingefuata kile ambacho mashirika ya kiraia, upinzani na Wakongo wengine walikuwa wakisema, hatungeweza kufikia hatua hii, "amesema Jean-Bosco Mambo, wa vuguvugu la kiraia lialodaia kuanzisha Upya kwa taifa, huku akitoa wito wa kuanzishwa kwa mazungumzo.

Tarehe 4 Agosti, Angola ilitangaza kusitishwa kwa mapigano, kufuatia majadiliano kati ya Kinshasa na Kigali. Vyanzo vya karibu na M23 vilitangaza kwamba waasi walisema hawahusiki na makubaliano haya ya kusitisha mapigano, kwa kuwa hawakushauriwa.

Chanzo: www.tanzaniaweb.live