Afrika

Habari

Burudani

Michezo

Biashara

Live Radio

Nchi

Kijamii

Lifestyle

SIL

Covid-19 yapunguza uzazi wa mpango

B86c8752bd547d4a4285dbb12cf062d3 Covid-19 yapunguza uzazi wa mpango

Tue, 28 Sep 2021 Chanzo: www.habarileo.co.tz

KAIMU Mkurugenzi Mkuu wa Afya nchini Kenya, Patrick Amoth, amesema kumekuwa na upungufu wa matumizi ya njia za uzazi wa mpango nchini kutokana na mlipuko wa ugonjwa wa Covid-19 kutoka asilimia 44 mwaka 2019/2020 hadi asilimia 29.6 mwaka 2020/2021.

Akitoa maoni yake katika maadhimisho ya Siku ya Uzazi wa Mpango, Amoth alisema Wizara ya Afya inakusudia kuongeza utoaji wa huduma za uzazi wa mpango wakati wa janga la Covid-19 ili kuzuia mimba zisizotarajiwa.

"Nchini Kenya, matumizi ya njia za uzazi wa mpango miongoni mwa wanawake kama njia ya kupanga uzazi, yamekuwa kwenye kiwango cha juu kutoka asilimia 37.2 mwaka 2017/18 hadi asilimia 44 mwaka 2019/2020, lakini sasa yamepungua hadi asilimia 29.6 mwaka 2020/21, kutokana na janga hilo," alisema Amoth.

Hata hivyo, alibainisha kuwa, Kenya ni miongoni mwa nchi zinazoongoza katika matumizi ya njia za kisasa za uzazi wa mpango katika nchi za Afrika zilizo Kusini mwa Jangwa la Sahara.

Ripoti ya Takwimu za Idadi ya Watu ya Mwaka 2021, iliitaja Kenya kuwa nchi ya nne yenye matumizi zaidi ya asilimia 60 ya njia za kisasa za uzazi wa mpango miongoni mwa nchi za Kusini mwa Jangwa la Sahara baada ya Zimbabwe na Eswatini kwa asilimia 66 na Lesotho asilimia 65.

"Mwaka 2021, inakadiriwa kuwa matumizi ya uzazi wa mpango yataepuka zaidi ya mimba zisizotarajiwa milioni 2.4 na vifo vya akina mama vinavyoweza kuzuilika 6,100," alisema.

Mwaka wa 2020, sindano zilikuwa njia ya kawaida ya uzazi wa mpango iliyotumiwa kwa asilimia 54.1, ikifuatiwa na kondomu za kiume (asilimia 13.8), vipandikizi (asilimia 13) na vidonge (asilimia 12.7).

Chanzo: www.habarileo.co.tz