Kituo Kudhibiti na Kuzuia Magonjwa CDC kanda ya Afrika kimeithibitishia BBC kwamba chanjo ya kwanza ya Mpox itawasilishwa DRC wiki hii.
Madaktari wanatarajiwa kuanza kutoa chanjo nchini humo,kitovu cha mlipuko huo ifikapo Ijumaa.
Shule nchini DRC zinatarajiwa kufunguliwa leo baada ya likizo, huku wazazi wengi wakitarajiwa kuwaacha watoto wao nyumbani huku kukiwa na wasiwasi wa idadi kubwa ya watoto walioathirika.
DRC inasema karibu wagonjwa 18,000 wa Mpox wamerekodiwa nchini humo, na vifo zaidi ya 600.
Wakati huohuo Kenya imeimarisha taratibu kwa wasafiri wanaoingia baada ya kurekodi mgonjwa wa nne wa Mpox.
Nchi hiyo itakusanya taarifa za mawasiliano kwa wote wanaowasili kutoka ng'ambo ili kusaidia kufuatilia mawasiliano iwapo kutatokea mlipuko.