MAMLAKA za afya Kaskazini mwa Zambia zimezindua kampeni ya chanjo ya ugonjwa wa kipindupindu, inayolenga kuzuia kuzuka mara kwa mara kwa ugonjwa huo katika wilaya.
Awamu ya kwanza ya kampeni ya chanjo hiyo, itafanyika wilaya ya Nsama ambayo ni moja ya wilaya zenye matukio mengi ya kipindupindu. Zaidi ya watu 7,000 watapewa chanjo hiyo.
Mratibu wa Taifa wa Kutokomeza Kipindupindu, Freddy Kapaya, alisema kuwa awamu ya kwanza, itafanyika kwa siku saba na chanjo hiyo itatolewa kwa watu wa umri wote, wakiwemo watoto wa kuanzia umri wa miezi 12.
Alisema baada ya hapo itafuata duru ya pili, ambayo itafanyika kwa siku 14. Alisema chanjo hiyo itakuwa na uwezo wa kufanya kazi ndani ya mtu kwa miaka mitatu.
Kapaya alisema wizara ya afya iliguswa kutokana na hatari kubwa inayosababisha ugonjwa huo kwenye baadhi ya wilaya.