SERIKALI ya Burundi imeamua kujizatiti katika kuimarisha maendeleo ya sekta ya Tehama kwa kuzindua mpango wa kuimarisha sekta hiyo hadi mwaka 2028 ambapo wawekezaji mbalimbali katika mifumo ya simu wataweza kuwekeza.
Hii itasaidia kuboresha shughuli za kiuchumi, kiutamaduni na za kijamii ambapo hatua za maendeleo zitapigwa katika sekta zote za binafsi na sekta za umma.
Kwa mujibu wa tangazo la Wizara ya Habari nchini humo, wawekezaji mbalimbali kutoka barani Afrika na Dunia kwa ujumla wataweza kuweka miradi yao mikubwa katika mfumo wa mawasiliano ya simu bila kupata tatizo lolote.
Baada ya mipango hiyo kukamilika, sekta ya Tehama inatarajiwa kuiingizia nchi kipato cha kutosha tofauti na ilivyo sasa hivi ambapo sekta hiyo haina pato la kutosha serikalini ingawa kuna idadi kubwa ya watumiaji wa simu za mkononi.
Ili kuondoa vikwazo mbalimbali vinavyosababishwa na miundombinu mibovu ya huduma za simu, serikali kwa kushirikiana na Benki ya Dunia imewekeza katika kuboresha mkongo wa taifa ambao utasaidia kuwa na mawasiliano bora.