Bunge la seneti la Nigeria limepitisha muswada wa adhabu ya kifungo cha miaka 15 jela kwa yeyote anayelipa fidia ili kumwachilia huru mtu ambaye ametekwa nyara.
Wakosoaji wanasema hatua hiyo si ya haki kwani inawafanya watu wanaotamani kuwaachilia huru jamaa zao kuhalalisha uhalifu kwa kushiriki.
Sheria hiyo mpya pia itatoa hukumu ya kifo au kifungo cha maisha jela kwa yeyote atakayepatikana na hatia ya utekaji nyara.
Kwa zaidi ya muongo mmoja, Nigeria imekuwa ikijitahidi kukabiliana na wimbi baya la utekaji nyara yanayofanywa na makundi yenye silaha ili kupata fedha.
Muswada huo unahitaji kujadiliwa na kupitishwa na bunge la chini kabla ya rais kutia saini kuwa sheria - mchakato ambao unaweza kuchukua wiki au miezi.