Afrika

Habari

Burudani

Michezo

Biashara

Live Radio

Nchi

Kijamii

Lifestyle

SIL

Bobi Wine aunda chama kipya kuelekea Uchaguzi

99d984764a82bc97fefd3b685a526d79 Bobi Wine aunda chama kipya kuelekea Uchaguzi

Tue, 28 Jul 2020 Chanzo: habarileo.co.tz

MWANASIASA wa upinzani nchini Uganda Robert Kyagulanyi maarufu Bobi Wine, amezindua chama kipya kinachojulikana kwa jina la National Unity Platform (NUP) kuelekea Uchaguzi Mkuu mapema mwaka 2021.

Kwa mujibu wa mwanasiasa huyo ambaye pia ni mwanamuziki wa Pop na mbunge wa jimbo la Kyandondo akiwa mgombea binafsi, chama hicho kipya kitakuwa chini ya vuguvugu aliloanzisha la People Power.

Hayo yanatokea ikiwa ni siku chache tangu chama tawala nchini Uganda cha NRM kumuidhinisha Rais wa nchi hiyo, Yoweri Museveni kugombea tena nafasi ya urais katika uchaguzi ujao.

Museveni anatarajiwa kukabiliana na Kyagulanyi katika uchaguzi ujao ambapo kwa mujibu wa wachambuzi wa masuala ya siasa nchini humo, kutakuwa na mchuano mkali kutokana na Kyagulanyi kuwavutia vijana walio wengi kutokana na sera zake za kuwapa ajira na kuwawezesha kupata fursa za kiuchumi.

Mwaka 2017 bunge la Uganda lenye wabunge wengi wa chama cha NRM, liliondoa ukomo wa umri wa rais, jambo lililokuwa kikwazo kwa rais Museveni kuwania tena kiti cha urais, na hivyo kumuwezesha kuwania urais.

Iwapo Rais Museveni atachaguliwa kuiongoza Uganda kwa muhula mwingine wa sita wa miaka mitano, atakuwa ameliongoza taifa hilo la Afrika Mashariki kwa miaka 40, na anaweza kuongoza miaka zaidi iwapo atataka kufanya hivyo.

Chanzo: habarileo.co.tz