Luanda, Angola. Mahakama Kuu nchini Angola, imemfungulia mashitaka ya ufisadi na ulaghai mwanamke tajiri Afrika.
Isabela dos Santos ambaye ni binti wa Rais wa zamani wa Angola, Jose dos Santos amefunguliwa mashitaka hayo leo Alhamisi Januari 23. Hata hivyo, kwa sasa binti huyo anaishi uhamishoni nchini Uingereza.
Kwa mujibu wa mashitaka hayo, Isabela anadaiwa kupora mali za taifa hilo kwa njia za kifisadi.
Akizungumza na waandishi wa habari, Mwanasheria mkuu wa Angola, Helder Pitta Groz alisema binti huyo wa rais wa zamani alifanya ufisadi wakati alipokuwa mwenyekiti wa kampuni ya mafuta ya Sonangol.
Pitta Groz alimtaka mwanamke huyo kujisalimisha haraka nchini Angola na kuyakabili mashitaka yake.
“Asipojisalimisha Mahakama itatafuta kibali cha kimataifa cha kumkamata yeye pamoja na watu wengine waliohusika katika ufisadi huo,” alisema mwanasheria huyo.
Habari zinazohusiana na hii
- Binti wa Rais Dos Santos azidi kubanwa
- Isabel dos Santos, mwanamke tajiri anayeandamwa kwa siasa, ufisadi
Alisema mwanamke huyo alitenda makosa hayo wakati alipokuwa mwenyekiti wa kampuni hiyo ya Sonangol.
Pitta Groz alisema makosa hayo yalibainika baada ya uchunguzi uliofanywa katika kampuni hiyo ya mafuta kwa kipindi cha miezi 18 kuanzia Juni, 2016.
Alisema uchunguzi huo ulianzishwa baada ya mrithi wa mwanamke huyo aliyetambulika kwa jina la Carlos Satumino kuileza mamlaka kuhusu uhamishaji wa fedha usio wa kawaida uliokuwa ukifanywa na Isabela.