BENKI Kuu imetoa noti mpya za paundi za Sudan Kusini 1,000 wakati uchumi wa nchi ukiwa unakabiliwa na changamoto nyingi zilizotokana na mlipuko wa ugonjwa wa covid-19, kupungua kwa bei ya mafuta katika soko la kimataifa na ufisadi uliokithiri.
Baada ya kutolewa kwa noti hizo, serikali imeweka mabango yenye picha za fedha hizo kwenye soko la Juba huku kukiwa na maneno yanayosomeka ‘Fahamu noti yako mpya.
Serikali ilianzisha noti ya paundi 1,000 ikiwa ni karibu mwaka mmoja sasa tangu iliposema itaanzisha noti mpya.
Wananchi wamepokea hatua hiyo kwa mawazo tofauti, baadhi yao wakidai haitasaidia kwenye uchumi.
“Lengo letu ni kuoanisha muundo wa noti na hitaji la watu wanaotumia kwa shughuli zao za kila siku. Tunahitaji noti ambazo ni rahisi, zenye ubora wa hali ya juu, salama na zenye gharama nafuu,” alisema Gavana wa Benki Kuu, Dier Tong.
Alisema Julai, 2019, benki hiyo ilipanga kuanzisha noti za paundi 1,000 baada ya kufanikiwa kutoa noti za paundi 500 mwaka 2018.