Serikali ya Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo (DRC), imemuita nyumbani kwa mashauriano balozi wake wa nchini Kenya ikilalamikia hatua ya Kenya kukubali kuwa mwenyeji wa mkutano wa wapinzani wa Kinshasa.
Taarifa ya serikali ya Kinshasa iliyotolewa na Alain Tshibanda, msemaji wa Wizara ya Mashauri ya Kigeni ya nchi hiyo imesema, hatua hiyo imechukuliwa kutokana na kutofurahishwa na hatua ya Kenya ya kukubali nchi yake kutumiwa na aliyekuwa kiongozi wa tume ya uchaguzi CENI, Corneille Nangaa pamoja na kiongozi wa waasi wa M23, kutangaza kuzindua vuguvugu la kisiasa linalofahamika kwa jina la Alliance Fleuve Congo, AFC.
Kwa upande wake msemaji wa serikali Patrick Muyaya ameziambia duru za habari kwamba, haiwezekani nchi wanayoshirikiana nayo kutafuta amani, kuruhusu tukio hilo kufanyika katika ardhi ya nchi yake.
Kabla ya hatua hiyo, jana Wizara ya Mashauri ya Kigeni ya Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo ilimwita katikak makao makuu ya wizara hiyo balozi wa Kenya mjini Kinshasa na kumkabidhi malalamiko ya nchi hiyo dhidi ya hatua ya nchi yake.
Corneille Naanga akiwa jijini Nairobi
Aliyekuwa Mwenyekiti wa Tume ya Uchaguzi nchini DRC, Corneille Naanga akiwa jijini Nairobi Ijumaa ya juzi akiwa ameambatana na kiongozi wa kundi la Waasi la M 23 Betrand Bisimwa, alizindua vuguvugu hilo la kisiasa.
Vuguvugu hili limeundwa na baadhi ya vyama vya kisiasa vilivyoko nchini na nje ya nchi, mashirika ya kiraia pamoja na makundi mengine yenye silaha yanayosema kuwa yanapigania wananchi ambao wamechoshwa na ugumu wa maisha.