Balozi wa Tanzania nchini Kenya, Dk John Simbachawene amevitaka vyombo vya habari nchini humo kutoa taarifa zenye uhakika kuhusiana na Tanzania na kuacha kuripoti taarifa zitakazoleta hofu kwa watu.
Simbachawene ametoa kauli hiyo leo ofisini kwake Jijini Nairobi baada ya chombo kimoja cha habari nchini humo kuripoti taarifa za uwepo wa taharuki za ugonjwa wa Corona nchini Tanzania kitu alichosema sio kweli.
“Nawataka Watanzania kuendelea kuchukua tahadhari za COVID-19 kwakuwa nchi yetu imekuwa mstari wa mbele kuhakikisha wananchi wanafuata ushauri wa wataalamu wa afya na miongozo inayotolewa na Shirika la Afya Duniani (WHO)” amesema Simbachawene.
Aidha, Balozi huyo amewataka watanzania wanaotaka kwenda nchini humo kuhakikisha kuwa wana nyaraka zote muhimu zinazohitajika kwa mujibu wa Wizara ya Afya zinazohusiana na ugonjwa huo.