Mahakama ya Eldoret imemhukumu Fidel Ochieng kifungo cha miaka 3 gerezani au kulipa faini ya Ksh.100,000 sawa na takriban Tsh. Milioni 1.7 baada ya kukiri kutuma ujumbe wa matusi kwa aliyekuwa Mke wake Sharon Bwonya, kupitia simu yake ya mkononi.
Mwendesha mashtaka aliiambia Mahakama kuwa maneno aliyoyatumia Ochieng katika ujumbe huo, ambao pia uliwahusisha wazazi wa Sharon, yalikuwa ya kashfa ambayo karani wa Mahakama alishindwa kuyasoma hadharani.
Akijitetea mbele ya Jaji Nancy Barasa, mshtakiwa aliomba Mahakama imsamehe, akisema kuwa aliandika ujumbe huo kwa hasira alizozipata baada ya kugundua kuwa Mkewe, ambaye alidai kumpenda sana, alimwacha kutokana na ushawishi wa Wazazi wake.