MWANAMKE mmoja aliyefahamika kwa jina la Getrude Ngoma (26) wa mjini Ndola nchini Zambia, amempeleka mchumba wake mahakamani kwa kushindwa kumuoa baada ya kuwa naye kwenye mahusiano kwa muda wa miaka nane tena akiwa amemzalisha mtoto.
Getrude amesema amechoka kumvumilia mwanaume huyo aliyefahamika kwa majina ya Herbert Salaliki ambaye alimuahidi kumuoa na badala yake hajafanya hivyo kwa kisingizio cha kutomudu gharama za harusi wakati tayari amekwisha toa mahari.
Getrude ambaye anaishi kwa wazazi wake na tayari ameshazaa na mwanaume huyo mtoto mmoja, ameongeza kuwa amechukua uamuzi huo baada ya kuona meseji za mchumba wake anazowasiliana na mwanamke mwingine hivyo kuingiwa na wasiwasi juu ya uaminifu wa mwanaume huyo.
Jaji Evelyn Nalwize ambaye ameisikiliza kesi hiyo katika Mahakama ya Jimbo la Kabushi, Ndola alimshauri Getrude kumaliza madai ya tofauti zao nje ya mahakama.
Chanzo: Daily Mail