MWANACHAMA wa Simba aliyetoka Mkoani Kigoma kwa mguu mpaka Dar es Salaam, Michael Philemon amewataka Wanasimba kujitokeza kwa wingi kuisapoti timu yao katika mchezo wa Jumamosi.
Mnazi huyo aliyetumia siku 15 kutoka Kigoma hadi Dar es Salaam amesema amevunja rekodi ya mwenzake wa Yanga aliyetumia siku 22.
Akizungumzia mchezo huo Michael Philemon amesema ni siku ya wanasimba kujitokeza kwa wingi wakiamini wanashinda mchezo huo muhimu katika msimu huu.
"Mimi Sina wasiwasi na kikosi changu najua naamini kitafanya vizuri katika mchezo huo, "amesema na kuongeza kuwa kitendo cha kutembea siku zote hizo ni kutokana na mapenzi yake ya dhati na Simba.
Aidha Philemon anawataka wanasimba wengine kuthubutu kufanya Kama yeye kutokana na mapenzi yao kwa timu yao pendwa ambayo inalitangaza Taifa na Afrika Mashariki kwa ujumla.
Amesema anawashukuru wanasimba wote waliojitolea kumpa hifadhi hapa Dar es Salaam ikiwemo kundi la Simba ushirikiano ambao wamekaa nae siku zote hizo.
"Simba kweli nguvu moja maana wamenipokea na tuko Kama ndugu mpaka nimejisikia vizuri Sana na kujiona siko mpweke hata kidogo, "
Katika kumpa sapoti shabiki huyo Manara alimpa sh 100,000 Kama motisha kwa kazi aliyoifanya kwa kujitolea na kwa mapenzi ya dhati.
"Mimi sikukuona lakini nakupongeza Sana kwa kujitoa kwako kutoka Kigoma Hadi Dar kwa mguu sio mchezo huu ni zaidi ya mzalendo, "amesema Manara
Imeandikwa na CLEZENCIA TRYPHONE NA DAUDI ELIBAHATI