Mahakama nchini Ufaransa imemhukumu kifungo cha maisha jela aliyekuwa afisa wa polisi wa Rwanda, baada ya kumpata na hatia ya mauaji ya halaiki na uhalifu dhidi ya binadamu.
Uhalifu wa Philippe Hategekimana ulifanyika wakati wa mauaji ya halaiki ya Rwanda mwaka 1994, wakati wanamgambo wa Kihutu walipoua mamia ya maelfu ya Watutsi na Wahutu wenye msimamo wa wastani.
Waendesha mashtaka walimweleza kuwa alikuwa na sehemu kuu katika kutekeleza mauaji hayo, sio tu kuua watu lakini pia kuwachochea wengine kufanya hivyo.
Hategekimana, ambaye alifanya kazi kama jenda mkuu huko Nyanza, mji ulioko kusini mwa nchi hiyo, alikimbilia Ufaransa baada ya mauaji ya kimbari.
Alipata hifadhi ya ukimbizi na utaifa wa Ufaransa chini ya jina la Philippe Manier.
Alifanya kazi kama mlinzi wa chuo kikuu nchini Ufaransa na alikimbilia Cameroon mnamo 2017 aliposikia malalamiko yamewasilishwa dhidi yake, AFP inaripoti. Alikamatwa Yaoundé na kurejeshwa Ufaransa mwaka uliofuata ili kushtakiwa.
Ilikuwa ni kesi ya tano ya aina hiyo nchini Ufaransa kwa mshukiwa mshiriki katika mauaji ya halaiki. Mauaji ya takriban Watutsi 800,000 na Wahutu wenye msimamo wa wastani yalifanyika kwa muda wa siku 100 mwaka 1994