Addis Ababa. Tanzania imetaka Umoja wa Afrika (AU) na Jumuiya za Kimataifa kuongeza jitihada na nguvu ili kuleta amani katika maeneo yenye migogoro barani Afrika hususani nchi za Burundi na Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC).
Hatua hiyo itaipunguzia Tanzania mzigo wa wakimbizi ulioubeba kwa muda mrefu hivi sasa.
Hayo yamesemwa leo Jumapili Februari 9, 2020 na Makamu wa Rais wa Tanzania, Samia Suluhu Hassani katika siku ya kwanza ya mkutano wa 33 wa kawaida wa Wakuu wa Nchi na Serikali wa Umoja wa Afrika unaofanyika Addis Ababa nchini Ethiopia.
Amesema kauli mbiu ya mkutano wa mwaka 2020 kunyamazisha silaha umekuja wakati muafaka kwa kuwa mapigano na kutokuwapo utulivu katika baadhi ya nchi za Afrika zinachelewesha maendeleo katika bara hilo.
Samia amesema endapo Umoja wa Afrika na Jumuiya za Kimataifa zitaongeza nguvu katika kunyamazisha silaha na kukawapo amani na utengamano ni dhahiri viongozi wataelekeza nguvu kubwa katika maendeleo endelevu ya wananchi hivyo kupunguza umasikini katika bara la Afrika ambalo linaonekana kama bara lililogubikwa na migogoro na mapigano.
Samia ameuahidi Umoja wa Afrika kuwa Tanzania itatekeleza kwa kasi mpango wa Umoja huo katika mapambano dhidi ya malaria na kwamba Tanzania imedhamiria kuutokomeza kabisa ugonjwa wa Malaria ifikapo mwaka 2030.
Pia Soma
- Basi lateketeza mizigo ya abiria 40, madereva wawili wafariki ajalini Morogoro
- Benki ya NBC yakabidhi msaada walioathirika na mafuriko Lindi
- Watoto watatu wa familia moja wafa maji wakiogelea