Mkuu wa Baraza la Utawala wa Mpito na Kamanda Mkuu wa Jeshi la Sudan, Abdel Fattah Al-Burhan, amesema kwamba hatafanya mazungumzo na Vikosi vya Msaada wa Haraka (RSF) maadamu vita vinaendelea.
Al Burhan amewaambia maafisa wa jeshi na askari katika eneo la kijeshi la Wadi Saydna huko Omdurman, magharibi mwa Khartoum kwamba: "Hatutafanya mazungumzo na RSF maadamu vita bado vinaendelea, na hatuko tayari kuzungumza na kundi hilo maadamu kuna uvamizi wa nyumba za raia katika miji ya El Geneina, Nyala, Zalingei, Al Daein (eneo la Darfur, magharibi mwa nchi), Khartoum na Al Jazira.”
Al-Burhan ameongeza kuwa: "Ikiwa waasi wanataka kufanya mazungumzo, lazima kwanza waondoe majeshi yao nje ya miji hii na kuyakusanya katika maeneo maalumu."
Ameongeza kuwa: "Tumejitolea kwa jukwaa la Jeddah, lakini upande mwingine lazima utekeleze majukumu yake, kulingana na kile kilichotiwa saini huko Jeddah."
Al Burhan alikuwa akiashiria mazungumzo ya Jeddah kati ya jeshi la Sudan na Vikosi vya Msaada wa Haraka, Mei 11, yaliyopelekea kupatikana makubaliano ya kwanza kati ya pande hizo mbili yanayosisitiza kulinda raia.
Mkuu wa Baraza la Utawala wa Mpito amesisitiza kuwa "kila mtu amedhamiria kuangamiza waasi wa RSF.