Mwanaume mmoja nchini Kenya Boniface Mutua mwenye miaka 47, ameishangaza mahakama ya Eldoret baada ya kukiri kuvuta bangi na kusema anafanya hivyo kumuunga mkono mgombea Urais nchini humo Prof. George Wajackoyah.
George amekuwa kivutio nchini Kenya hasa kwa sera yake anayosisitiza kuhalalisha kilimo cha bangi kwa ajili ya kukuza uchumi
Mbele ya Hakimu Mkazi Mwandamizi Christine Menya, mtuhumiwa huyo alidai anatumia bangi kama kichocheo, na kumuunga mkono mgombea urais anayempenda Prof. George Wajackoyah.
Mutua ambaye alikiri mashtaka yanayomkabili, alidai kuwa bangi inamsukuma kuwa na ujasiri na nguvu ya kumfanyia kampeni Wajackoyah.
Mutua alikamatwa katika shamba la Bahati huko Ainabkoi, kaunti ya Uasin Gishu, baada ya kupatikana na roli tatu za bangi zote zenye thamani ya sh90 za Kenya
Hakimu alilisisitiza kuwa ni kinyume cha sheria za Kenya kumiliki au kuvuta bangi nchini Kenya hivyo mtuhumiwa ana kesi ya kujibu. Kesi hiyo itaendelea Julai 27, 2022.