Watu tisa wamefariki papohapo akiwemo mtayarishaji wa Muziki kutoka Puerto Rico, Jose Angel Hernandez ama Flow La Movie baada ya ndege binafsi waliyokuwa wakisafiria kuanguka nje ya mji mkuu wa Jamhuri ya Dominika, Santo Domingo.
Taarifa ya Shirika la Ndege na vyombo vya habari vya ndani vimesema ajali hiyo imetokea Jumatano na kwamba ilikuwa na wafanyakazi wawili na abiria saba. Ilikuwa ikitikea katika uwanja wa ndege wa El Higuero kuelekea Miami hata hivyo muda mchache iliomba kutua katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Las Americas uliopo Santo Domingo.
Hapakuwa na maelezo mengine ikiwa ni pamoja na sababu za rubani kubatilisha safari ama chanzo cha ajali.
Kufuatia tukio hilo, uwanja wa ndege ulifunga shughuli zake, na kufuta mamia ya safari za ndege.
Vyombo vya habari vya ndani vilisema mpenzi wa Hernandez na mwanawe walikuwa miongoni mwa waliofariki, na kwamba wawili kati ya waliofariki walikuwa watoto wa umri wa miaka minne na 13.