Afrika

Habari

Burudani

Michezo

Biashara

Live Radio

Nchi

Kijamii

Lifestyle

SIL

Afisa wa Somalia anaonya mpango wa ATMIS

Afisa Wa Somalia Anaonya Mpango Wa ATMIS Afisa wa Somalia anaonya mpango wa ATMIS

Wed, 5 Jul 2023 Chanzo: Voa

Naibu Rais wa Jubaland, eneo ambalo majeshi ya Kenya na Ethiopia yanaendesha shughuli zake ameiambia VOA Idhaa ya Ki-Somali kuwa itakuwa vigumu kwa vikosi vya Somalia, kuhakikisha kuna usalama, katika maeneo ambako vikosi vya Umoja wa Afrika vinaondoka

Wakati kikosi cha mpito cha Umoja wa Afrika nchini Somalia kinachojulikana kama ATMIS kikipunguza idadi ya wanajeshi, afisa mmoja wa Somalia anaonya kwamba mpango huo haukubaliki na unaongeza hatari ya wanamgambo wa al-Shabab kuyatwaa maeneo waliyopoteza.

Naibu Rais wa Jubaland, eneo ambalo majeshi ya Kenya na Ethiopia yanaendesha shughuli zake ameiambia VOA Idhaa ya Ki-Somali kuwa itakuwa vigumu kwa vikosi vya Somalia, kuhakikisha kuna usalama, katika maeneo ambako vikosi vya Umoja wa Afrika vinaondoka.

Kutakuwa na hatari kutoka huko, Mohamud Sayid Aden alisema Jumanne. Adui atapata faida. Raia ambao walivitegemea vikosi vya Somalia na ATMIS watakuwa na wakati mgumu wa kulipiziwa kisasi kutoka kwa wanamgambo wa al-Shabab.

Ujumbe wa kulinda amani wa Umoja wa Afrika nchini Somalia umekamilisha kukabidhi kambi sita za kijeshi kwa vikosi vya Somalia wiki iliyopita. Kituo cha saba kilifungwa.

Umoja wa Afrika unataka kupunguza hatua kwa hatua idadi ya wanajeshi hadi Desemba mwaka 2024, wakati muda wa ujumbe huo utakapokamilika.

Kupunguzwa kwa wanajeshi 2,000 ambapo 400 kutoka kila nchi tano zinazochangia wanajeshi hao, Burundi, Ethiopia, Djibouti, Kenya na Uganda kutafanya idadi ya wanajeshi hao kupungua hadi 16,586.

Umoja wa Afrika umekubaliana na serikali ya Somalia kuondoa wanajeshi wengine 3,000 ifikapo mwishoni mwa mwezi Septemba.

Ni mpango ambao haujafikiriwa vizuri, ni wa haraka, Aden alisema.

Aden alitoa wito wa kusitishwa na kufanyiwa tathmini kuhusu kupunguzwa wanajeshi hao.

Lakini maafisa wengine wa Somalia walitofautiana. Yasin Abdullahi Mohamud, anayejulikana kama Farey ni mbunge, na mkurugenzi wa zamani wa Shirika la Taifa la Upelelezi na Usalama. Kwa sasa ni miongoni mwa maafisa wanaohamasisha vikosi vya ndani dhidi ya al-Shabab.

Anasema Wasomali wanashukuru vikosi vya AU lakini uamuzi wa kupunguza vikosi sio jambo linalotakiwa kufanywa kwa haraka.

Ni wakati mwafaka kwa vikosi kuondoka, alisema. Ni muhimu kwa jeshi la taifa kuchukua jukumu la usalama.

Mohamud alisema vikosi vya ATMIS havikuhusika kwa kiasi kikubwa katika operesheni za kijeshi dhidi ya al-Shabab ndani ya kipindi cha mwaka jana na alisisitiza wakati umefika kwa vikosi vya Somalia kuchukua hatua.

Kupunguzwa kwa vikosi vya AU kunakuja wakati ambapo serikali kuu inajiandaa kuanza tena operesheni za kijeshi dhidi ya al-Shabab, harakati ambazo zilikatizwa na mvua pamoja na mashambulizi ya wanamgambo yanayosababisha vifo.

Chanzo: Voa