KOCHA Mwinyi Zahera wa Yanga ameshangazwa na umbali wa kutoka Tanga mpaka Singida kiasi cha kusema mpira wa Tanzania ni ngumu kuendelea. Akizungumza na Mwanaspoti, alisema ratiba yao imekuwa ngumu baada ya kusafiri kwa umbali huo na kisha kurejea tena Tanga kwaajili ya mchezo dhidi ya JKT Tanzania.
"Kutembea masaa 15 kwenda kucheza mechi ni mara yangu ya kwanza maishani kukutana nayo, tukitoka hapa tunatakiwa turudi tena Tanga kwa staili hii ni ngumu mpira wa Tanzania kuendelea, timu zinapata wakati mgumu sana," alisema.
Akizungumzia mchezo wao dhidi ya Singida, alisema mchezo huo utakuwa mgumu na wa kutumia nguvu lakini atatumia wachezaji wengine ili kupata ushindi.
"Inabidi nibadili kikosi kwa ajili ya mchoko wa wachezaji, tunataka tupate ushindi japokuwa michezo iliyopita ilikuwa migumu na kutumia nguvu nyingi," alisema.
Aliongeza kwamba marefa wanatakiwa kuchezesha mpira kwa haki bila kuwa upande wowote ule.