YANGA imefuzu nusu fainali Kombe la Shirikisho la Azam (ASFC) baada ya kuifunga Mwadui FC mabao 2-0 katika mchezo wa robo fainali uliochezwa Uwanja wa CCM Kambarage Shinyanga jana.
Kwa matokeo hayo Yanga itakutana na Biashara United ya Mara katika mchezo wa nusu fainali utakaochezwa kwenye Uwanja wa Ali Hassan Mwinyi Tabora. Biashara iliingia hatua hiyo baada ya kuifunga Namungo kwa mabao 2-0.
Iliwachukua dakika 25 Yanga kuandika bao la kwanza lililofungwa na Deus Kaseke baada ya kuuwahi mpira uliokuwa kwa kipa wa Mwadui Mussa Mbisa aliyejaribu kumchenga mchezaji huyo na kujikuta akifanya makosa na mfungaji akaunasa na kuutumbukiza nyavuni.
Bao hilo lilidumu hadi kipindi cha kwanza na kuifanya Yanga kuwa mbele ya 1-0.
Kipindi cha pili timu zote zilirejea kwa kasi na kuichukua Yanga dakika 11 kupata bao la pili dakika ya 56 lililofungwa na Kaseke akipokea pasi ya kichwa kutoka kwa Yacouba Songne.
Yanga ilikuwa inashambulia lango la wapinzani kwa asilimia kubwa na kutengeneza nafasi nyingi kwa vipindi tofauti ila walikosa umakini.
Pia Mwadui baada ya kushindwa kufunga kwa mipira ya karibu walikuwa wanapiga mipira mirefu langoni kwa Yanga lakini kipa Farouk Shikalo alikuwa makini na kuikoa.