SIMBA itawasili Jumatano keshokutwa ikitokea kambini Afrika Kusini na Agosti 3 ,wachezaji na viongozi wa klabu hiyo watatembelea hospitali ya Ocean Road kutoa msaada kuelekea Tamasha la Simba Day litakalofanyika Agosti 6 Uwanja wa Taifa.
Mtendaji Mkuu wa Simba Crensetius Magori amesema Julai 31 wataaanza wiki ya Simba na siku hiyo watasaini mkataba wa miaka miwili na mdhamini wa jezi na vifaa vya mazoezi na Kisha kuzizindua jezi hizo.
"Siku ya Julai 31 tutaingia mkataba na kuzindua jezi zetu za nyumbani na ugenini na tutatangaza sehemu zitakapouzwa nchi nzima.
"Agosti Mosi tutazindua kadi za benki zitakazojulikana kama Smart Card ambazo zitamuwezesha mwanachama atakayekuwa nayo kuwa na akaunti ya benki husika kupitia kadi hiyo.
"Agosti 3 wachezaji watatembelea hospitali ya Ocean Road kutoa misaada mbalimbali wagonjwa kama tulivyofanya Muhimbili mwaka uliopota.
"Tunaomba siku hiyo ya Agosti 3 wanachama,wapenzi na mashabiki wa Simba nchi nzima wajitokeze katika hospitali mbalimbali kutoa misaada kwa watu wasiojiweza Kama sehemu ya kurudisha kwa jamii" alisema Magori.
Magori alisema siku ya kilele Cha Simba Day Agosti 6 kutakiwa na mechi tatu, kwanza watacheza Simba Queens, kisha timu ya vijana ya timu hiyo halafu timu ya wakubwa ya Simba itacheza na Power Dynamo ya Zambia.