MSHAMBULIAJI Mbwana Samatta wa timu ya Taifa Tanzania na klabu ya KRC Genk, ametangazwa kuwa mshindi wa tuzo (Eboy Shoe Award 2019) ya mchezaji bora wa mwa Kiafrika anayecheza nchini Ubeligiji.
Baada ya kuchukua tuzo hiyo, imemfanya nyota chipukizi wa Serengeti Boys, Kelvin John ‘Mbappe’ akubali mziki wa Samatta ambao ameuonyesha msimu huu katika Ligi Kuu ya Ubeligiji.
Mbappe baada ya kupata taarifa za Samatta kupata tuzo hiyo, alisema kwa namna ambavyo amepambana (Samatta) ana kila sababu ya kupewa tuzo bila kikwazo chochote.
“ Hongera sana kwake na kiukweli alistahili kuchukua hii tuzo kwa kitu ambacho amekionyesha msimu huu, amepambana na kila mtu ameona nini ambacho amekifanya,” alisema.
Mbappe aliongeza kupitia kwa Samatta amejifunza kuongeza nidhamu katika kazi pamoja na kujituma muda wote ili kufika katika lengo ambalo amejiwekea.