Usiku wa Ulaya unarejea tena leo kwa miamba ya kijerumani The Bavarians Bayern Munich watawaalika klabu ya benfica ya ureno kwenye uwanja wa Allianz Arena huku taarifa njema zikiwa uwezekano wa kurejea kwa kocha Julian Nagelsmann ambaye alipata uviko 19 wiki mbili zilizopita.
Bayern kwenye michezo mitatu, wamefunga magoli 12 bila ya wavu wao kuguswa huku wakiwa na alama tisa huku wakihitaji alama tatu pekee kuwapeleka hatua 16 bora .
Barcelona yenye alama tatu itakuwa nchini Ukraine kupambana na Dynamo Kiev yenye alama moja ambapo kufungwa kwao na wababe wa catalunya leo usiku kutafuta matumaini ya kuelekea 16 bora.
Barca Chini ya kocha wa mpito Sergi Barjuan itakosa huduma ya nyota wake Sergio Aguero 33, ambaye atakuwa nje ya uwanja kwa miezi 3 kutokana na matatizo ya kifua huku mlinzi Gerard Pique akikosekana kwa tatizo la kifundo cha mguu.
Ingawaje taarifa njema kwa Barcelona ni kujumuishwa Kwa wachezaji waliokuwa majeruhi Ousmane Dembele, Ansu Fati, Frenkie de Jong na mlinzi Ronald Araujo kwenda kupambana na Dynamo Kiev.
Kundi F ambalo bado halitatoa timu mapema kwenye mzunguko wa nne, itashuhudia vita ya kufufua matumaini ya kuelekea 16 bora kwa nyambizi ya njano klabu ya Villarreal yenye alama (4) kuwakaribisha Young Boys yenye alama (3) kutokea Uswizi.
Kwingineko Stadio di Bergamo sasa ukijulikana kama Gewiss stadium,Atalanta yenye alama 4 itawakaribisha mashetani wekundu Manchester United yenye alama 6 huku nyota wa kireno, Cristiano Ronaldo akirejea kwa mara ya kwanza Italia baada ya kucheza misimu mitatu na kunyakua makombe mawili ya ligi kuu nchini humo maarufu kama Scudeto alipokuwa na Juventus.
Atalanta katika michezo 9 ya UCL nyumbani wameshinda michezo 3,sare 3 na kufungwa michezo 3 huku michezo 26 waliocheza kwenye michuano ya ulaya wakicheza michezo 26 na kushinda michezo 13,sare michezo 9 na kupoteza michezo 4.
Huku Meneja wa Atalanta, Gian Piero Gasperini akinukuliwa kuelekea mchezo wa leo akihuzunishwa kwa kuondoka kwa Ronaldo nchini italia akisema angetamani kumuona angesalia kwenye Seria A kwa sababu ni mchezaji mkubwa .
United wanaingia Stadio de Bergamo wakiwa na rekodi ya kucheza katika ardhi ya Italia mara 20 na kushinda kwenye michezo 6, sare kwenye michezo 3 na kufungwa mara 11.
Huku kwa United itaakuwa mara yao ya 24 kucheza hatua ya makundi huku mara 18 wakivuka hatua ya 16 bora na kuweka rekodi ya kuwa kinara kutokea England ingawaje msimu wa 2020/21 wakishindwa kuvuka baada ya kushika nafasi ya tatu.
Mchezo wa leo utakuwa ni mchezo wa 180 kwa Cristiano Ronaldo akiendeleza rekodi yake mwenyewe ya kucheza michezo mingi ndani ya UCL huku anayemfuata ni Iker Casillas aliyecheza michezo 177.
United chini ya Ole Gunnar Solskjear kwenye michezo 10 iliyopita ya mashindano yote waliocheza wamefungwa katika michezo 5,sare moja na kushinda michezo 4,swali kubwa likisalia kwa Solskjear kama atavuka viunzi vilivyopo mbele yake? Tusubirii
Michezo mingine kundi G, Sevilla watakuwa nyumbani kuwakaribisha lille ya ufaransa ilhali kwenye dimba la Volkswagen Arena,wenyeji Vfl Wolfsburg watawakaribisha Salzburg yenye alama 7 ambapo ushindi kwenye mchezo wa leo kwa Salzburg utawapeleka kwenye 16 bora.
Wakati michezo ya mwisho kwa leo kundi H, Malmo ya Sweden watawakaribisha mabingwa watetezi Chelsea the blues huku taarifa njema ni kurejea kwa kiungo Christian Pulisic baada ya kukosekana tangu mwezi wa 8 kutokana na majeraha ya kifundo cha mguu huku miamba hiyo ya darajani wakiendelea kukosa huduma za nyota Mason Mount, Romelu Lukaku, Timo Werner pamoja na kiungo Mateo Kovacic.
Juventus chini ya Massimiliano Allegri wao watahitaji alama tatu kufuzu kwenda 16 bora watakapokuwa nyumbani kuwakabili Zenith St Petersburg ya Urusi huku kibibi kizee cha turin wakiwa na alama 9 wakifunga magoli 5 bila wavu wao kutikiswa.