KIUNGO wa Azam FC na Taifa Stars, Salum Abubakar 'Sure Boy' ambaye alifunga bao la ushindi katika mchezo dhidi ya Guinea ya Ikweta amesema ana imani Stars itacheza Fainali za Afcon 2021 zitakazofanyika nchini Cameroon.
Hayo aliyazungumza mara baada ya kumalizika kwa mchezo huo wa kwanza wa makundi uliochezwa uwanja wa Taifa jijini Dar es Salaam na kwamba huu ni muda wake kwenda Afcon.
"Sikucheza Afcon zilizopita, kwahiyo natamani kucheza Afcon safari hii, naamini kila kitu kinawezekana," alisema.
Sure Boy katika mchezo huo alifunga bao la ushindi baada ya kupiga shuti kali akipokea pasi Ditram Nchimbi na kwenda moja kwa moja wavuni.
Stars iliibuka na ushindi wa bao 2-1 na sasa wanatarajia kucheza mchezo wao wa pili dhidi ya Libya utakaochezwa Novemba 19 nchini Tunisia.
Mchezo huu unachezwa Tunisia badala ya Libya baada kuwepo na machafuko ya kivita nchini Libya.