Michezo

Habari

Burudani

Biashara

Afrika

Live Radio

Nchi

Kijamii

Lifestyle

SIL

Siwa, Mmachinga kuiongoza Yanga Kagame

6e778002adc58de36022c34233347b9a Siwa, Mmachinga kuiongoza Yanga Kagame

Fri, 30 Jul 2021 Chanzo: www.habarileo.co.tz

UONGOZI wa klabu ya Yanga umempa kocha wa makipa Razak Siwa, jukumu la kuiongoza timu hiyo kwenye michuano ya Kombe la Kagame katika nafasi ya Kocha Mkuu akisaidiwa na wachezaji wa zamani wa timu hiyo Fred Mbuna na Mohamed Hussein ‘Mmachinga.

Michuano hiyo inatarajiwa kuanza kutimua vumbi Agosti mosi, Uwanja wa Benjamini Mkapa huku Yanga ambao ni mabingwa mara tano wa taji hilo wakipangwa kundi C pamoja na timu za Express ya Uganda na Nyasa Bullets ya Malawi.

Akizungumza na gazeti hili jana, Makamu Mwenyekiti wa Kamati ya Mashindino ya Yanga, Injinia Hersi Said alisema wamempa Siwa kazi hiyo kutokana na kocha wao Mkuu na wasaidizi wake kwenda mapumziko baada ya msimu kumalizika.

“Tunaimani na Siwa pamoja na wasaidizi wake Mbuna na Mmachinga, kama kamati tutatoa sapoti yote kuhakikisha Siwa na wasaidizi wake wanafanya vizuri ili kuendelea kuimarisha rekodi ya timu yetu kwenye michuano hiyo,” alisema Injinia Hersi.

Kiongozi huyo alisema, kuhakikisha timu yao inafanya vizuri kwenye michuano hiyo, wamependekeza kuwatumia wachezaji saba kutoka kikosi cha timu ya wakubwa akiwemo kiungo kutoka Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo Mukoko Tonombe, na wachezaji wengine ambao hawakupata nafasi ya kucheza mara kwa mara.

Wachezaji hao saba wakikosi cha kwanza ni Said Juma ‘Makapu’, Wazir Junior, Mapinduzi Balama, Abdallah Shaibu ‘Ninja’, Poul Godfrey, Yassin Mustapha na kipa chaguo la tatu Ramadhan Kabwili.

Hersi alisema kupitia michuano hiyo wanatarajiwa kuwatambulisha wachezaji wawili wazawa ambao waliowasajili kwa ajili ya msimu ujao ambao ni David Bryson kutoka KMC na winga Dickson Ambundo kutoka Dodoma Jiji.

Kwa mujibu wa ratiba ya Kagame, Yanga itaanza kampeni zake Agosti 2 dhidi ya Express na baadae Nyasa Big Bullets.

Aidha kiongozi huyo amethibitisha klabu hiyo kuachana na nahodha wake Lamine Moro, baada ya mjadala mrefu na kufikia makubaliano hayo ambapo Yanga watalazimika kumlipa mshahara wa Julai na Agosti.

“Nikweli tumeachana na beki nahodha wetu Lamine Moro lakini kwa makubaliano ya pande zote mbili na sisi kama uongozi tunamshukuru kwa mchango wake mkubwa tangu alipojiunga na sisi na tunamtakia mafanikio mema huko anakoelekea,” alisema Hersi.

Beki huyo aliyewahi kufanya majaribio kwenye kikosi cha Simba kabla ya kusajiliwa na Yanga kwa mapendekezo ya Kocha Mwinyi Zahera, amekuwa na tatizo la utovu wa nidhamu kiasi cha kutokuwa na maelewano mazuri na kocha wake Nasreddine Nabi, ambaye aliwahi kumsimamisha kabla ya kumrudisha zikiwa zimebaki mechi mbili kumaliza.

Chanzo: www.habarileo.co.tz