Shinyanga. Timu ya Simba imeondoka na alama tatu kwenye mchezo wake wa Ligi Kuu dhidi ya Stand United Uwanja wa Kambarage mkoani Shinyanga.
Mabao ya Simba yalifungwa na John Bocco kipindi cha pili, huku wakiendelea kushikilia nafasi ya tatu baada ya kufikisha alama 51.
Yanga ndio wanaongoza kileleni wakiwa na alama 64 na wakifuatiwa na Azam FC nafasi ya pili yenye pointi 53.
Stand United walipambana kuhakikisha wanapata bao lakini safu ya ushambuliaji ya Simba iliyoongoza na Bocco kisha kuingia Meddie Kagere iliwavuruga wapinzani wao.
Awali, pamoja na kwenda mapumziko kwa timu zote bila kufungana,washambuliaji wa Simba walikosa nafasi kadhaa.
Wachezaji,Adam Salamba,Rashid Juma na John Bocco licha ya kuisumbua ngome ya Stand United,lakini walikosa umakini katika kuzitumia vyema nafasi walizopata katika kipindi cha kwanza.
Mabeki wa Stand United wakiongozwa na Kimbondile walikuwa mwiba kwa kuwazuia washambuliaji wa Simba.
Mbali na hayo ,Simba ilipata pigo baada ya Straika wake, Salamba kushindwa kuendelea na mchezo baada ya kuumia na nafasi yake kuchukuliwa na Meddie Kagere.
Salamba alipelekwa hospitali ya Mkoa wa Shinyanga kwa matibabu zaidi.