Inaweza kufika wakati unaingia uwanjani ukauliza Simba wako upande gani, kutokana na kile kinachoelezwa kuwa, Katiba ya klabu hiyo inaruhusu timu hiyo kuvaa rangi zaidi ya nyekundu na nyeupe.
Kwa miongo kadhaa, Simba imekuwa ikitumia rangi mbili tu, nyekundu na nyeupe, lakini juzi akizungumza na Wahariri, Kaimu Rais wa Simba, Abdallah Salim ‘TryAgain’ amesema kuwa wakati wowote wakipata mdhamini akaja na mapendekezo yake, Simba itayafuata ikiwemo kubadili rangi ya jezi kwa wakati maalumu.
Amesema kuwa anafahamu kwamba Simba ina rangi zake, lakini Katiba nayo kipo kipengele kinaruhusu katika eneo hilo kufanya ambavyo itaonekana inafaa kwani matakwa ya mdhamini yana nafasi yake.
TryAgain amesema wanachama lazima wakubali mabadiliko kwani hata timu ya taifa ya Brazil, imezoeleka kuwa na rangi ya njano na bluu, lakini wakati mwingine wanakuwa na bluu tupu.
Amesema kingine kinachowasukuma kuliona hilo ni kwamba klabu mbalimbali za Ulaya zina nafasi ya kuwa na sare ya jezi za aina tatu, kuna ya nyumbani, ugenini na nyingine ambayo inaweza kuamliwa vinginevyo.
Simba imekuwa katika mchakato wa mabadiliko mbalimbali kuelekea kwenye Simba Kampuni ambayo zaidi ni kuhakikisha Simba inafikia kule kunakotakiwa na kila mwanachama.