Dar es Salaam. Simba inaendelea na ratiba ngumu ya mechi mfululizo na sasa inatinga Kanda ya Ziwa ikiivaa Kagera Sugar leo kwenye mchezo wa Ligi kuu Bara utakaofanyika kwenye Uwanja wa Kaitaba Bukoba.
Timu hiyo haina budi kupambana na hali yake kucheza mechi mfululizo kila baada ya siku moja au mbili ili kwenda sawa na timu nyingine ambazo ziko mbele kwa mechi tisa na kuhakikisha mechi zinamalizika Mei kama ilivyopangwa awali.
Baada ya mchezo na Kagera Sugar, Simba itapumzika siku moja na Jumatatu itaikabili Alliance kwenye Uwanja wa CCM Kirumba Mwanza na April 25 itacheza na Biashara United kwenye Uwanja wa Karume Mara.
Ratiba hiyo inaonekana kumchanganya kocha wa Simba, Aussems Patrick ambaye alieleza kushangazwa na ratiba hiyo huku timu yake ikitakiwa kusafiri mkoa mmoja kwenda mwingine lakini kubwa akihoji vipi kuhusu afya za wachezaji ikiwa mechi zinakaribana hivyo.
Katika michezo 10 ya hivi karibuni ambayo Kagera Sugar imecheza imeshinda miwili tu huku ikipoteza sita na kutoka sare michezo miwili na iko nafasi ya 17 kwenye msimamo wa ligi ikiwa na pointi 36.
Hata hivyo Kagera Sugar itakuwa na kazi kubwa kupambana na Simba ambayo imekuwa na rekodi bora dhidi ya timu hiyo iwe nyumbani na ugenini
Katika mechi nne ambazo Simba imecheza kwenye Uwanja wa
Kaitaba tangu 2015 imeshinda tatu na kupoteza moja
matokeo ambayo ni sawa na mechi nne ilizocheza kwenye
Uwanja wa Taifa.
Simba ilipoteza mchezo dhidi ya Kagera kwenye Uwanja wa Kaitaba, April 4, 2017 mchezo ambao uliwatibulia Wekundu wa Msimbazi katika mbio zao za ubingwa kuwaacha watani zao Yanga wakichukua kilaini.
Jambo hilo liliwaumiza Simba na kulipa kisasi msimu ulipita kwa kuichapa Kagera Sugar mabao 2-0 kwenye uwanja huo hivyo leo ni jambo la kusubiri kuona nani atamsimamisha mwenzake huku Kagera ikishangilia kurudia kwa wachezaji wake watatu George Kavila, Edward Christopher na Ramadhan Kapera waliokuwa majeruhi.
Simba yenye pointi 60 inaingia katika mchezo huo ikiwa na rekodi bora kwenye Ligi Kuu kwani tangu Novemba 23 mwaka jana ilipotoka suluhu na Lipuli baada ya hapo imeshinda michezo yake yote 11 iliyofuata.
Kagera Sugar inabidi iingie kwa tahadhari leo kuikabili Simba ambayo inaonekana haitanii kwani katika michezo hiyo 11 iliyoshinda iliwafunga pia wapinzani wake wakubwa katika mbio za ubingwa Yanga na Azam.
Kikosi hicho cha kocha Mecky Maxime hakina mwenendo mzuri kwenye ligi hivyo lazima wapambane katika kushinda michezo yao sita iliyobaki ukiwemo wa leo dhidi ya Simba ili kujinasua na janga la kushuka daraja.
Kocha wa Kagera Sugar, Mecky Maxime alisema: “Tunajua tuko katika nafasi mbaya kwenye msimamo wa ligi hivyo tumejiandaa kushinda mchezo wa kesho (leo) .
Kocha wa Simba, Patrick Aussems alisema licha ya kwamba ratiba inawabana lakini watapambana kuhakikisha malengo yao ya kutwaa ubingwa msimu huu yanatimia ukichangiwa na pointi tatu za Kagera.
“Ratiba imekuwa sio rafiki kwetu lakini tutapambana hivyo hivyo huku tukifanya mzunguko wa wachezaji wote kwa ajili ya kuhakikisha kila mechi tunashinda,” alisema Aussems.