Moja ya viungo bora kwenye kikosi cha Mwadui ya Shinyanga ni Abdallah Seseme mwenye uwezo wa kufunga na kutengeneza mabao kwenye kikosi hicho.
Kiungo huyo mshambuliaji aliyezaliwa Oktoba 29, ameweka wazi chimbuko la kipaji chake, namna ya uchezaji wake na mengineyo katika mazungumzo na jarida hili la Spoti Mikiki.
Kipaji
Seseme anasema namna ambavyo kipaji chake kilivyoibuliwa na Sifa United ya Manzese jijini Dar es Salaam.
“Kipaji changu kilianza kunolewa kwenye timu ya Sifa United ya Manzese maeneo ya tip top, ilikuwa mwaka 2005 na baadaye Simba ambapo ilikuwa 2009 nilianzia ngazi ya chini B ambayo ilinifanya kujua vitu vingi vya kimpira”anasema Kiungo huyo ambaye alizaliwa mwaka 1993.
Wachezaji wapo wa aina tofauti na kuna wakati mwingine hubadilika kutokana na majukumu kwa upande wake anaelezea namna yake ya uchezaji.
“Nimekuwa nikicheza kwenye nafasi ya kiungo mshambuliaji ambaye huwa nawajibika kwenye kutengeneza nafasi wakati mwingine ikitokea huwa nafunga, sasa hutegemea upande ambao kocha anaweza nipanga kucheza”anasema Seseme.
Biashara
Upande wa baishara na kwenyewe Seseme yumo. Mchezaji huyo wa zamani wa Simba anasema amekuwa akijishulisha na ufanyaji wa biashara mbalimbali ambazo zimekuwa zikisaidia kuendesha maisha yake.
“Ninabishara zangu ambazo zinanifanya niwe naingiza kipatao kwa njia nyinge, Mpira utabaki kuwa kazi yangu kuu ambayo hata hivyo itafika kikomo lakini upande wa biashara nitaendelea,”anaeleza Seseme.
Magari
Seseme amekuwa mfuatiliaji mzuri wa aina za magari na anasema aina ya gari ambalo anatamani kuwanalo.
“Napenda sana magari na siwezi ficha maana natamani siku moja kuwa na Toyota Altezza, ni gari fulani hivi lenye mvuto wa aina yake ambalo binafsi huwa sichoki kulitizama” anasema.