UBWABWA, ubwabwa, ubwabwa… walisikika wakiimba maelfu ya mashabiki wa Yanga waliojitokeza kwenye Uwanja wa Mkapa jijini Dar es Salaam kushuhudia kilele cha Wiki ya Mwananachi. Shangwe hizo zilinogeshwa na Mgombea Urais kupitia Chama cha CHAUMA, Hashimu Rungwe ambaye amepata umaarufu kwa ‘Mzee wa Ubwabwa’
Japokuwa maswali yaliyoibuka miongoni mwa mashabiki ambayo hayakuwa na majibu, ni je Rungwe naye ni shabiki wa Yanga au alikuja pale kwa lengo la kupiga kampeni, maana aliwahi kuahidi kuwa kampeni zake atakuwa akizifanya kwenye mikusanyiko ya watu.
Rungwe mwenyewe alisema kuwa ni shabiki mkubwa wa Yanga toka akiwa mdogo na kwamba alikwenda kushuhudia wachezaji wapya walioshushwa kwenye klabu hiyo.
“Naipenda Yanga na nataka ifanye vizuri, Nangoja kuona vitendo baada ya kusajili… Tuna majeraha ya kipigo cha juzi juzi cha kufungwa na Simba bao 4-1. Sasa Yanga inatakiwa kuifunga Simba bao sita au saba ili tufurahi,” alisema Rungwe.