Mshambuliaji wa simba, Emmanuel Okwi raia wa Uganda huenda akawa amefika visiwani Zanzibar wakati wenzake wakiwa kwenye boti kuelekea huko baada ya yeye kuondoka na usafiri wa anga.
Kikosi kizima cha Simba chini ya Mbelgiji Patrick Aussems kimeondoka kwa usafiri wa maji lakini Okwi ambaye sio jasiri wa kutumia usafiri huo imeelezwa ameondoka na Ndege.
Hii si ajabu kwa mashambulizi huyo mwenye mabao tisa kwenye ligi kuu Bara kutumia usafiri huo kuelekea Zanzibar kwa kile kilichoelezwa anaogopa kusafiri kwenye maji.
Tangu ajiunge Simba wanapoweka kambi yao visiwani humo basi sio rahisi kumuona Okwi akiwa na wenzake ndani ya boti wakielekea huko.
Mwanaspoti ambalo linaenda kupiga kambi visiwani humo liligundua kutokuwepo kwa mshambuliaji huyo kwenye msafara na kuelezwa kuwa ameondoka na Ndege.
Miaka michache iliyopita kabla ya Okwi kwenda kucheza Denmark kulikuwepo na malalamiko ya mchezaji huyo kupendelewa kupanda Ndege lakini ilifafanuliwa kuwa ni muoga kutumia usafiri wa maji na hawezi kabisa.