HALI ilikuwa si hali ndani ya Uwanja wa Uhuru jijini Dar es Salaam katika mchezo kati ya Yanga na Iringa United wa Kombe la Shirikisho baada ya kundi kubwa la nyuki kuvamia uwanjani hivyo kuleta taharuki kwa wachezaji, wamauzi na mashabiki.
Kundi hilo la nyuki lilipita uwanjani dakika ya 53 na kuwafanya wachezaji wa timu zote mbili pamoja na wamauzi kulala chini.
Baada ya wachezaji kulala, beki wa Yanga Ali Mtoni Sonso alionekana kunyanyuka ghafla huku akijikung'uta kichwani akiashiria kung'atwa na wadudu hao hivyo kukimbia nje kwenye benchi la timu yao ili kpata huduma ya kwanza.
Nyuki hao hawakuishia uwanjani tu kwani walienda mpaka katika baadhi ya majukwaa na kusababisha mashabiki kulala chini na wengine kukimbia kujiokoa.
Tukio hilo lilidumu kwa dakika sita na dakika ya 59 mwamuzi aliashiria mchezo kuendelea baada ya hali kuwa sawa na nyuki hao kutokomea.