Dar es Salaam. Nyota wa Simba waliokuwa katika kikosi cha timu ya Taifa ya Tanzania 'Taifa Stars' wameripoti na kuanza mazoezi huku kiungo Jonas Mkude akifika wakati wenzake wakiwa wamemaliza mazoezi kwenye Uwanja wa Boko Veteran, Dar es Salaam.
Wachezaji wa Simba waliokuwa katika kikosi cha Taifa Stars kilichoichapa Uganda na kufuzu kwa Afcon 2019 ni Aishi Manula, John Bocco, Erasto Nyoni na Mkude.
Katika mazoezi ya leo asubuhi Nyoni, Bocco na Manula waliocheza dhidi ya Uganda walifika mapema mazoezini hapo na kuungana na wenzao.
Mkude ambaye hakucheza dhidi ya Uganda alifika mazoezini na kuwakuta wenzake wakiwa wamemaliza mazoezi.
Kiungo huyo alifika mazoezini hapo akiwa amevalia mavazi yanayotumika na timu ya Taifa Stars.
Beki Mganda Jjuuko Murshid ni mchezaji pekee wa kigeni aliyekuwa katika timu ya taifa aliyefika katika mazoezi hayo.
Nyota mwingine Emmanuel Okwi (Uganda), Zana Coulibaly (Burkina Faso), Clautos Chama (Zambia) na mshambuliaji Meddie Kagere wote hawakuwepo katika mazoezi ya leo asubuhi.