Michezo

Habari

Burudani

Biashara

Afrika

Live Radio

Nchi

Kijamii

Lifestyle

SIL

Nyoshi: Nitafia dansi

Nyoshi Pic Data Nyoshi: Nitafia dansi

Sat, 22 May 2021 Chanzo: www.mwanaspoti.co.tz

NDANI ya gemu ya muziki wa dansi kwa zaidi ya miaka 30, staa wa muziki huo Nyoshi El Saadat anaendelea kubamba na ametamba kuwa atafia kwenye kuupambania muziki huo.

Licha ya kushiriki kufanya muziki wa kizazi kipya, ikiwamo aliposhirikishwa na MwanaFA katika wimbo wa Gwiji uliomhusisha pia Maua Sama, Nyoshi anasisitiza kwamba kamwe hatauacha muziki wa dansi ambao umepitia katika vipindi vya kupanda na kushuka.

Kwa sababu ya muziki huu, Nyoshi alikaa rumande pamoja na wanamuziki wenzake kadhaa wa Kicongo wa iliyokuwa bendi ya FM Musica kutokana na sakata la vibali vya kuishi na kufanya kazi nchini na walipotoka waliachia ngoma iliyotingisha sana ya ‘Prison (Jela ni Mbaya),’ baadaye wakaunda FM Academia hadi sasa yuko na bendi yake mwenyewe ya Bogoss Musica.

Akiwa na Bogoss, staa huyo ataongoza mapambano ya kuurejesha katika chati zake muziki wa dansi katika tamasha kubwa la kila mwaka la muziki huo linalokwenda kwa jina la Wafia Dansi, ambalo mwaka huu litafanyika Mei 29 kwenye Ukumbi wa Terminal Pub, mjini Morogoro. Tamasha hili litakutanisha bendi zaidi ya tano na wanamuziki wa kujitegemea kutoka kote Tanzania.

Baadhi ya bendi zitakazotumbuiza ni Bogoss, Waluguru Original kutoka Morogoro chini ya Killer Boy, Sky Melodies kutoka Dodoma chini ya Nico Milimo, Gold Musica kutoka Dodoma chini ya Yamodo ‘Mr. Utamu’ na mwanamuziki wa kujitegemea, Jimmy Manzaka ‘Mfalme wa Rhumba’.

Tamasha la Wafia Dansi hufanyika kila mwaka katika miji tofauti ambapo kwa mara ya kwanza lilifanyika 2018 Mzalendo Pub, Dar, na mwaka 2019 lilifanyika Villa Park Mwanza na 2020 halikufanyika kutokana na janga la Corona.

Chanzo: www.mwanaspoti.co.tz