Sare zimeendelea kutawala katika mechi za Ligi Kuu Bara inayowakutanisha Yanga na Namungo baada ya leo pia timu hizo kutoka sare ya bao 1-1.
Mabao ya Obrey Chirwa na Saido Ntibazonkiza yamefanya timu hizo kufikisha mechi tano za Ligi Kuu Bara tangu 2019 bila yoyote kuwa mbabe wa mwenzake.
Chirwa aliipatia Namungo bao dakika ya 52 kwa shuti Kali lililomshinda kipa wa Yanga, Diarra.
Dakika ya 59 Yanga ilifanya mabadiliko ya wachezaji watatu kwa mpigo baada ya kuwatoa Mukoko Tonombe, Jesus Moloko na Farid Mussa na kuwaingiza Said Ntibazonkiza 'Saido', Deus Kaseke na Yusuph Athuman lakini dakika tano baadae wakamtoa Kibwana Shomari na kumuingiza David Brayson wakati kwa upande wa Namungo alitoka Shiza Kichuya na nafasi yake kuchukuliwa na Hashim Manyanya.
Licha ya kufanya mabadiliko hayo Yanga haikuonekana kubadilika kiuchezaji huku Namungo wakilinda lango lao kwa nidhamu wakiongozwa na mabeki Baraka Mtui na Abdul Malick.
Hata hivyo dakika ya 78, Namungo ilipata pigo baada ya kiungo wake mkabaji, Hashim Nyenye kuonyesha kadi nyekundu na mwamuzi, Abel William wa Arusha kwa kumfanyia madhambi Feisal Salum' ' Fei Toto' katika eneo la hatari.
Faulo hiyo pia ilizaa penalti kwa Yanga iliyofungwa dakika ya 81 na Saido na kuamsha shangwe kwa mashabiki wa timu hiyo waliokuwa kimya muda mwingi wa mchezo
Katika mchezo huo kipa wa Yanga Diarra anastahili sifa kwa kuzuia timu yake isipoteze mchezo kwani aliweza kuokoa hatari nyingi golini kwake kutokana na safu yake ya ulinzi kukatika mara kwa mara.
Dakika ya 47 Diarra alifanya kazi nzuri kwa kupangua shuti la Shiza Kichuya aliyekuwa ameshawapita mabeki na kuelekea kufunga lakini pia kipa huyo raia wa Mali alifanya kazi safi dakika ya 69 kwa kuokoa shuti la Hashim Manyanya akitizamana nae.
Katika mchezo huo wachezaji wa Namungo, Baraka Mtuwi na Hashim Nyenye walionyeshwa kadi za njano wakati kwa upande wa Yanga aliyepata kadi ni Djuma Shaban na Saido.