Nahodha na mshambuliaji wa klabu ya Lipuli ya mkoani Iringa, Paul Nonga ameomba radhi kwa uongozi wa klabu hiyo na sasa amerejeshwa katika kikosi cha wanapaluhengo hao ambacho kimeanza harakari za kujikwamua na janga la kushuka daraja.
Mshambuliaji huyo wa zamani wa vilabu vya Mbeya City na Yanga, mkataba wake ulimalizika Julai mosi mwaka huu, aligoma kurejea kikosini akishinikiza kulipwa madai yake ya fedha za usajili na mshahara.
Kocha wa timu hiyo Nzeyimana Mailo amesema Paul Nonga, Novaty Lufunga na Seif Karihe wote wameomba radhi na wao kama walezi wamewaelewa hivyo wapo kikosini na anatarajia watatoa mchango katika mechi tatu zilizosalia.
Lipuli iliifunga KMC mabao 2-0 na kujitoa katika mstari wa kushuka daraja na sasa wanashughuli nzito ya kuzikabili Yanga, Azam na Ruvu Shooting ili wajihakikishie wanasalia ligi kuu msimu ujao.