Dar es Salaam. Shirikisho la Riadha Tanzania (RT), limemuengua mwanariadha Gabriel Geay kwenye timu ya Taifa, iliyotarajiwa kuondoka leo alfajiri kwa mafungu kwenda Nigeria kushiriki mashindano yatakayoanza kesho kwenye mji wa Asaba.
Katibu Mkuu wa RT, Wilhelm Gidabuday alisema Geay ameachwa kutokana na mazingira ya kumtoa Marekani kwenda Nigeria kushiriki mashindano hayo.
Gidabuday alisema kundi la kwanza la msafara huo litaondoka Uwanja wa Ndege wa Kilimanjaro (KIA) saa 9:00 alfajiri na wengine wataondoka Dar es Salaam (JNIA) saa 10:00 alfajiri kwenda Kigali, Rwanda.
Msafara huo hautakuwa na kiongozi zaidi ya kocha Christian Matembo, ukiwa na wanariadha Failuna Abdi na Augostino Sulle anayekimbia mbio za mita 5,000 na 10,000, Michael Gwandu kuruka juu na Ali Gullam mita 100 na 200.