TIMU ya Soka ya Mtibwa Sugar inawazia namna ya kupata pointi sita ili kuwa na uhakika wa kubaki Ligi Kuu.
Kikosi hicho kinachonolewa na Kocha Mkuu Mohamed Badru kimejichimbia katika kambi yake Manungu kuhakikisha hakifanyi makosa kwenye mechi zilizobaki za kumaliza msimu.
Kocha Badru aliliambia gazeti hili kuwa wanahitaji kushinda angalau mechi mbili zijazo ili kuondoka katika presha ya kushuka daraja.
“Kila mchezo kwetu ni kama fainali, lakini bila kudharau mpinzani yeyote ni lazima tujipange kwa michezo yetu ijayo, tukishinda kuanzia mechi mbili kidogo tutapata unafuu na presha itapungua,”alisema.
Mchezo ujao Mtibwa inatarajiwa kucheza na Mwadui ugenini hivyo Badru alisema wanajipanga kuhakikisha mchezo huo wanafanya vizuri na kuzidi kujiweka pazuri.
Timu hiyo inayoshika nafasi ya 11 kwa pointi 34 haina uhakika wa kubaki kama itafanya vibaya katika michezo ijayo.
Lakini pengine tumaini lao litarejea chini ya Badru aliyejiunga nao siku za hivi karibuni kwani mwenendo wa mechi karibu tano zilizopita sio mbaya baada ya kushinda tatu na kupoteza mbiili.