Dar es Salaam. Kocha wa Simba B, Mussa Hassan Mgosi amesema kilichoibeba Simba kutinga robo fainali ya Ligi ya Mabingwa Afrika ni uzoefu wa baadhi ya nyota wa kikosi hicho.
Mgosi alisema idadi kubwa ya wachezaji wa kikosi cha kwanza cha Simba SC wamekuwa na uzoefu wa kutosha kwa kucheza michezo mbalimbali na mikubwa ya kimataifa.
“Kagere amekuwa akitegemea kwenye timu yake ya taifa pia kwa umri wake lazima uone ukomavu kwenye aina hii ya michezo, nilimuona Bocco akiwa kwenye kiwango cha juu pamoja na Okwi kipindi cha kwanza.
“Erasto na Wawa waliifanya Simba kuwa imara kwenye safu ya ulinzi pamoja na kuwa kulikuwa na makosa madogo madogo, pia nadhani watu walimuona Niyozima alivyoleta utofauti,” alisema.
Mshambuliaji huyo wa zamani wa Simba, alisema kocha wa kikosi hicho, Patrick Aussems anajukumu moja zito mbele yake kuhakikisha timu inakuwa na hesabu nzuri ya uchezaji wa michezo yan ugenini.
“Hatua ya mtoani ni tofauti na michezo ya makundi, ukipoteza mechi kwa idadi kubwa ya mabao unajiweka pabaya kwenye mchezo wa marudiano,” alisema Mgosi.