Baada ya kuibuka sintofahamu kuhusu ushindi wa Formula 1 kwa Max Verstappen, timu ya Mercedes imeamua kuachana na mpango wa kukata rufaa kupinga matokeo.
Mbio za Abu Dhabi ziligubikwa na ushindani mkali kati ya Lewis Hamilton na Max Verstappen kabla ya Verstappen kumpiku Hamilton kwenye mzunguko wa mwisho na kuibuka mshindi. Mercedes walianza kuibua hoja zao dhidi ya msimamizi wa mchezo huo ambapo, kama timu, hawakufurahishwa na uzingatiwaji wa sheria na kanuni za mchezo huo.
Kwa mujibu wa sheria za FIA, timu yeyote yenye pingamizi inapatiwa masaa 96 kukata rufaa. Ilidhaniwa Mercedes wangefanya hivyo baada ya uongozi wa timu hiyo na Hamilton mwenyewe kuonesha hadharani kutopendezeshwa na namna mbio hizo zilivyofanyika.
Hilo limekuwa tofauti baada ya timu hiyo kutoa tamko la uthibitisho kuwa, hawatofungua shauri lolote la kukata rufaa dhidi ya FIA na badala yake, wameingia kwenye majadiliano ya kheri yenye lengo la kuboresha zaidi usimamizi wa mchezo huo kwa siku zijazo.