Mechi kati ya Simba na JKT Tanzania iliyokuwa ifanyike leo Jumatano jioni imehairishwa kutokana na mvua kubwa kunyesha muda mfupi kabla ya mchezo huo.
Mechi hiyo iliyokuwa ichezwe kwenye Uwanja wa Jamhuri Morogoro imeshindwa kufanyika kutokana uwanja huo kujaa maji.
Timu zote mbili zilifika uwanjani hapo kama kawaida lakini zikashindwa kufanya mazoezi ya kupasha misuli moto kutokana na mvua kuendelea kunyesha.
Licha ya waamuzi,kamisaa wa mchezo na timu hiyo kusubiri dakika 15 ili kuona kama hali hiyo itabadilika lakini hali ya uwanja kujaa maji ilionekana sio rafiki kwa wachezaji kuutumia uwanja huo kwa mechi.
Baada ya uamuzi hiyo Simba ndio alikuwa wa kwanza kupanda katika basi na kuondoka wakifuatiwa na JKT Tanzania.
Katibu wa Chama cha Soka Mkoa wa Morogoro(MRFA),Charles Mwakambaya ambaye pia ni msimamizi wa kituo cha Morogoro amesema wameamua kuhairisha mchezo huo kutokana na uwanja maji.
"Tumeamua tuhairishe mchezo kwa sababu tumeona uwanja hautafaa kucheza kwa sababu umejaa maji.Awali tulisubiri kidogo kuona labda maji yangekauka lakini yakaendelea kuwepo uwanjani.
"Kwa kanuni za ligi kii mechi ilikuwa ichezwe kesho Alhamis lakini tumeiangalia na Simba mabayo inamechi ya kimataifa Jumamosi na kwa mujibu wa kanuni za Shirikisho la Soka Duniani(Fifa),timu inataka icheze mechi moja kwenda nyingine baada ya masaa 72 hivyo kama mechi ingeruhusiwa kuchezwa Alhamis tungekuwa hatujaitendea haki Simba"amesema Mwakambaya.
Mwakambaya amesema kwa mashabiki waliolipa viingilio kwa ajili ya kutazama mchezo huo watawafanyia utaratibu mzuri wa kuona nini watafanya kwa kushirikiana na Shirikisho la Soka Tanzania(TFF).