Mbeya. Mbeya Kwanza imeendelea kujifua kwa ajili ya Ligi Kuu msimu ujao baada ye leo Ijumaa kuichapa bao 1-0 Ihefu katika mechi ya kirafiki iliyopigwa wilayani Mbarali mkoani hapa.
Katika mchezo kila Kocha alifanya mabadiliko kwa kuwachezesha nyota wake ili kubaini ubora na udhaifu.
Ikumbukwe Mbeya Kwanza inajiandaa na Ligi Kuu ilhali Ihefu wakijinoa kwa ajili Championship baada ya kushuka daraja msimu uliopita.
Ihefu ambao walikuwa nyumbani walionekana kuzidiwa haswa kipindi cha kwanza licha ya kuweza kupambana kutoruhusu bao ndani ya dakika 45 za kwanza.
Kipindi cha pili timu zote zilifanya mabadiliko ya kikosi chote ambapo Ihefu walionekana kuelewana lakini walijikuta wakifungwa bao dakika ya 69 kupitia kwa Willy Edger aliyeipandisha Mbeya Kwanza akiwa mfungaji bora wa msimu uliopita alipofunga mabao 13.
Mchezo huo ulikuwa wa kwanza kwa Ihefu chini ya Kocha Zuberi Katwila, huku ukiwa wa sita kwa Mbeya Kwanza iliyo chini ya Mrundi, Haruna Hererimana ambao yote wameshinda.