Mbao imetinga nusu fainali ya mashindano ya SportPesa baada ya kuwafunga Mabingwa watetezi Gor Mahia ya Kenya kwa penalti 4-3. Ikishangiliwa uwanja mzima na mashabiki wa Simba na Yanga,Mbao ilionyesha kandanda safi hasa kipindi cha pili na kuwabana vilivyo wapinzani wao. Timu hizo zilikwenda hatua ya penalti baada ya dakika 90 kutoka sare ya bao 1-1. GorMahia ndio ilikuwa ya kwanza kufunga bao dakika ya 52 lililofungwa kwa Penalti na Dennis Oliech kabla ya Mbao kusawazisha dakika ya 76 kupitia kwa Raphael Siame. Mbao iliendelea kufanya mashambulizi lakini safu ya ulinzi ya Gor Mahia ilikuwa makini kuokoa hatari zote langoni kwao. Katika mikwaju ya penalti, Gor Mahia walifunga kupitia kwa Francis Kahata, JacquesTuyisenge ,na Boniface Omond wakati Harun Shakavah na Shafik Batambuze walikosa. Mbao ilifunga penalti zao kupitia kwa Said Khamis,Raphael Siame, Hamimu Abdukarim na David Mwasa wakati Hashimu Ibrahim alikosa.