STRAIKA Vitalis Mayanga ameamua kuweka wazi usajili wake dhidi ya Simba kwamba haupo na ni mchezaji huru baada ya kumaliza mkataba wake Ndanda FC ya Mtwara.
Mayanga alitajwa kusaini mkataba na Simba wakati wa dirisha dogo Mashindano ya Caf ilipokuwa inashiriki Ligi ya Mabingwa lakini baadaye hakujiunga nao na kuendelea kuitumikia Ndanda.
Sababu kubwa iliyomfanya Mayanga ashindwe kuitumikia Simba ni kutokana na muda wa usajili wachezaji wa ndani kumalizika ambapo dirisha lilikuwa limefungwa.
Jana Ijumaa, mmoja wa Wajumbe wa Bodi ya Wakurugenzi wa Simba, alisema usajili wa Mayanga umekatiliwa na kocha wa Patrick Aussems kwa madai kuwa kiwango chake hakina tofauti na baadhi ya wachezaji alionao, hivyo anahitaji mchezaji wa tofauti.
Kupitia ukurasa wake wa Instagram, Mayanga aliamua kuweka wazi kwamba hajasaini mkataba timu yoyote hivyo yeye ni mchezaji huru.
"Asante Mungu wangu kwa kumaliza ligi salama, kwasasa nimemaliza mkataba wangu Ndanda FC na sina mkataba na timu yoyote, niko tayari kufanya makubaliano na yoyote atakayekuwa tayari, Mungu naomba niongoze,".
Msimu uliopita alikuwa na mchango mkubwa katika kikosi chake kutokana na uwezo wake wa kupambana na mabeki huku akimaliza ligi akiwa amefunga mabao 10, mabao yake yalikuwa na mchango mkubwa kwa kuiwezesha Ndanda kumaliza nafasi ya saba.