KOCHA wa Polisi Tanzania, Seleman Matola amesema michezo mitatu ya kirafiki am,bayo timu yake imecheza ameridhishwa na viwango vya wachezaji wake hasa eneo la beki na kiungo, akipanga kutumia muda uliobaki wa maandalizi kuwanoa washambuliaji wake ili timu hiyo iweze kuvuna mabao mengi kwenye Ligi Kuu Bara.
Polisi Tanzania ambayo imepanda dajaja kucheza Ligi Kuu Bara msimu ujao imeshacheza michezo mitatu ya kirafiki dhidi ya KMC, Azam na Ndanda na ikashinda miwili na kupoteza mmoja.
Matola ambaye amejiunga timu hiyo mwaka huu akitokea Lipuli ya Iringa amesema maandalizi ya ligi yanakwenda vizuri kwa timu yake isipokuwa bado hakuna muunganiko mzuri kwa washambuliaji wake.
"Ukiangalia kuanzia mabeki mpaka viungo wanacheza vizuri hakuna tatizo ila upande wa ushmbuliaji bado hakuna maelewano na ushirikiano mzuri, hivyo katika muda huu uliobaki kabla ya ligi kuanza tutatumia nafasi hiyo kurekebisha na kuhakikisha safu ya ushambuliaji inacheza kwa ushirikiano ili tuweze kupata mabao mengi kwenye ligi," amesema Matola.
Polisi Tanzania itacheza tena mchezo wa kirafiki kesho Jumamosi dhidi ya Namungo Fc kwenye Uwanja wa Majaliwa , mchezo ambao utatumika kwa Namungo kutambulisha wachezaji wake watakaotumika msimu ujao.