Baada ya kutambulishwa Yanga na kuanza kufanya mahojiano na vyombo vya habari, Haji Manara ametoa Sh700,000 kwaajili ya kumchangia mshambuliaji wa Polisi Tanzania Gerald Mdamu aweze kupatiwa matibabu.
Manara ambaye sasa anaenda kuwa kwenye timu ya uhamasishaji Yanga amechanga hela hiyo kumsaidia Mdamu ambaye alipata ajali na timu yake wakati akitoka mazoezini kujiandaa na mechi za mwisho wa msimu ulioisha na kuvunjika miguu yote.
“Kiasi hicho nilichokitoa naamini kitasaidia kwa sehemu kufanikisha matibabu nawapongeza nahodha wa zamani wa Yanga, Ally Mayai na wa sasa wa Simba John Bocco kwa kupigania suala la Mdamu, watanzania wengine wajitokeze kufanikisha hili,” amesema.
Manara aliongeza kuwa atakuwa mmoja wa Watanzania ambao wataendeleza kampeni ya kumchangia Mdamu ili aweze kurudi kwenye hari yake ya kawaida. Mdamu alihamishiwa Hospitali ya Taifa Muhimbili kwa matibabu zaidi.