NYOTA wawili wa kikosi cha kwanza cha Mwadui FC, Beki Iddy Mobby ‘Kiraka’ na Winga kushoto Mathias Gerald wataukosa mpambano wa kesho Alhamisi wa Ligi Kuu dhidi ya Yanga kutokana na kuwa majeruhi.
Mwadui itakuwa na kibarua kizito pale watakapowavaa Yanga katika mtanange wa Ligi Kuu utakaopigwa kwenye Uwanja wa Kambarage mjini Shinyanga.
Meneja wa timu hiyo, Daud Hassani alisema Mobby anasumbuliwa na maumivu ya mbavu huku Gerald akisumbuliwa na majeraha ya goti ambapo amesema ndio wachezaji watakaikosa mechi hiyo.
“Niseme tu katika huu mchezo tutawakosa Mobby na Gerald ambao ni majeruhi hata hivyo tayari nafasi zao zimepata wachezaji wa kuziziba kwenye mpambano huo wa kesho,” alisema Hassani.
Hata hivyo Meneja huyo alisema wamejipanga kikamilifu katika mchezo huo ambao amesema ni muhimu kuweza kupata pointi tatu.
Alisema akuwa wanawaheshimu Yanga kutokana na rekodi waliyoiweka hadi sasa ya kucheza mechi 10 bila kupoteza, hivyo ushindi wao wa leo utaweka historia ikiwemo kuwafunga kwa mara ya kwanza katika Ligi Kuu msimu huu.
“Ni kweli matokeo yetu si mazuri sana kama wapinzani wetu na ndio maana tunataka kushinda ili kujiweka nafasi nzuri,lakini tuweke rekodi mpya ya kuwafunga kwa mara ya kwanza kwa sababu hawajapoteza mechi yoyote,” alisema Meneja huyo.