LEO Jumamosi, Kamati ya Utendaji ya Shirikisho la Soka Tanzania TFF) itakutana kujadili mambo mbalimbali ukiwa ni utaratibu kwa mujibu wa katiba huku suala la mabadiliko ndani ya Bodi ya Ligi (TPLB), ambapo majina ya Crescentius Magori (pichani chini) na Almas Kasongo yakitajwa kuchukua nafasi ya mtu ndani ya bodi hiyo.
Habari kutoka ndani ya TFF, zilizopenyezwa kwa Mwanaspoti zinasema mabadiliko yanayoendwa kufanywa ndani ya TFF na TPLB ni kwenye nafasi ya ofisa mtendaji wa bodi inayoshikiliwa kwa sasa na Boniface Wambura anayeelezwa anarejeshwa ndani ya shirikisho.
Kama mabadiliko hayo yatafanywa imeelezwa kwamba Wambura atakuwa mkuu wa kitengo cha habari na masoko ambapo atasaidiana na Aaron Nyanda na Cliford Ndimbo.
Hata hivyo, kwa mujibu wa taratibu za ajira ndani ya shirikisho hilo, likifanya mabadiliko hayo litatakiwa kutangaza ajira ya mtendaji mkuu wa Bodi ya Ligi ambapo watakaoomba watatakiwa kufanyiwa usajili ingawa miongoni mwa watu wanaotajwa kushika nafasi hiyo ni mtendaji mkuu wa zamani wa Simba, Crescentius Magori au akawa Mwenyekiti wa Chama cha Soka Mkoa wa Dar es Salaam (DRFA), Almas Kasongo.
“Kesho (leo) kuna kikao cha kamati ya utendaji kitajadili mambo mbalimbali ingawa mabadiliko hayo yanaweza kujadiliwa pia,” kilisema chanzo hicho.
Mwanaspoti lilimtafuta ofisa habari wa TFF, Ndimbo ambaye alikiri kuwepo kwa kikao hicho, lakini juu ya mabadiliko hayo alisema hayafahamu.
Pia Soma
- Mechi ya Pyramids: Mbinu tano za kuibeba Yanga
- Miraji kumrejesha Okwi Msimbazi?
- Sean, Matty: Ndugu waliokamata kiungo cha Newcastle United EPL
Hata hivyo, Magori alipotafutwa na Mwanaspoti kutaka kuthibitisha taarifa hizo za kutajwa kuwa bosi wa TPLB, alisema: “Siyo kweli, niliongoza TFF miaka ya nyuma kama makamu wa rais (kipindi cha Leodegar Tenga) na sijawahi kufikiria kwenda kuongoza Bodi ya Ligi. Kama ni kurudi kwenye mpira basi niwe rais wa TFF na sio huko, presha ya bodi ya ligi haina tofauti na presha ya kuiongoza klabu kama ya Simba au Yanga.”
Hata hivyo, chanzo hicho cha ndani ya TFF kimesisitiza kuwa Magori ndiye anayekuja kuwa mtendaji mkuu wa Bodi ya Ligi na kama akichomoa basi anayechukua nafasi hiyo ni Kasongo ambaye ana uzoefu mkubwa na pilikapilika za soka la Tanzania.